Dec 17, 2013

SOMA HAPA UIMARISHE NDOA YAKO



Takriban katika maisha ya wanandoa walio wengi kama sio wote, ndoa zao hupitia katika vipindi tofauti. Kama ulivyo umri wa Binadamu, ndoa hupitia katika kipindi cha utoto, ujana na uzee, na kila kipindi kina mambo yake na taratibu zake kama tulivyoona katika makala iliyopita ambazo kama wanandoa watashindwa kuzifuata basi huenda ndoa hiyo ikakumbwa na mtihani mkubwa, nao ni mtihani wa kuchokana.

Hivyo basi, sababu kubwa ya wanandoa kuchokana, au kuzeeka kwa ndoa kunasababishwa na mwanamke, pale ambapo atashindwa kutumia nafasi yake na vipawa alivyopewa kuleta utulivu katika ndoa yao, na katika makala yetu ya mwanzo tulianza kuangalia baadhi ya visababishi vinavyopelekea katika kuchokana kwa wanandoa.
Leo InshaAllaah tutaendelea kuangalia na kuchambua visababishi vengine ambavyo ni muhimu kwa wanandoa kuvielewa, hususan mwanamke.
d-    Kutamka na kudhihirisha mapenzi: Ni muhimu sana kwa wanandoa ili kuyaimarisha mapenzi yao yasiote mvi, kutamkiana hisia zao za kupendana bila utangulizi wowote, kwa mume au mke kumwambia mwenzake NAKUPENDA kuna athari nzuri katika nafsi kuliko hata ungemletea zawadi ya kitu cha gharama. Na Mtume wetu (Swalla Allaahu  ‘alayhi wa aalihi wa sallam) ametufundisha haya kwa kusema:
(Atakapompenda mmoja wenu ndugu yake basi amfahamishe, kwani huzidisha maelewano na kuthibitisha mapenzi) Hadiyth Sahihi, Silsilatus Swahiyhah
Haya ni mafundisho ya Kiislamu ambayo leo hii yanaonekana ni mila za kimagharibi, na huonekana kioja katika jamii mke kumwambia mumewe kuwa ‘Nakupenda’ na si ajabu mume mwenyewe au mke anayeambiwa hivyo na mwenzake akajibu kwa hayaa “ Ah hebu acha utani wako, sisi tumeishazeeka”. Lakini wanandoa wengi hupenda kudhihirisha mabaya na mambo yanayowakera kuliko yale mazuri ya kufurahisha, jambo ambalo kwa kiwango kikubwa linachangia katika kuchokana haraka.
e-    Kupeana zawadi: Zawadi ni njia nzuri ya kudhihirisha mapenzi yako  na nafasi ya mwenzako katika maisha yako, na zawadi ambayo mtu huitoa kwa mwenzake bila ya utangulizi au mnasaba maalum huleta athari njema na huimarisha mapenzi, kama tulivyofundishwa na Mtume wetu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) katika  Hadiyth aliyosimulia Abu Hurayrah:(Peaneni zawadi mtapendana) Ibn Hajar Al-‘Asqalaaniy
Na katika zoezi hili la kupeana zawadi, ni vema kila mmoja akaelewa anachokipenda mwengine ili zawadi iwe na athari inayotarajiwa, na iwe ni zawadi maalum kwa mlengwa, isiwe zawadi ambayo mtoaji naye atafaidika na zawadi hiyo, kwa mfano, si vema kwa mwanamme kumletea mkewe zawadi ya sufuria, microwave, pazia, Dinner set, hiyo haitaitwa zawadi, lakini ni juu yake kumletea manukato ayapandayo, hereni, bangili, mkufu au pete ya dhahabu, na vitu ambavyo ni maalumu kwa matumizi yake binafsi. Hali kadhalika kwa mwanamke kumzawadia mumewe achunge vigezo hivyo.
f-      Kualikana vyakula: Inaweza kushangaza kuwa vipi wanandoa wataalikana chakula wakati wenyewe ni mume na mke, na ni lazima wale pamoja?! Ni vema ikaeleweka kuwa, kubadili mazingira na kufanya vitu makhsusi kwa kushtukizana, huwafanya wanandoa  kutozoeana na kuchokana, kwani maisha yenye mtindo na mtiririko mmoja kila siku humfanya mtu kuyachoka, ni vema wanandoa na hasa mwanamke kuwa mbunifu katika kuyapaka rangi mpya maisha yao kwa kubuni vitu vitakavyo tia ladha mpya katika nyumba, njia  mojawapo ni hiyo ya kumualika chakula maalum mumewe peke yake, na hata kama itamlazimu kununua au kuagiza aina tofauti ya chakula basi afanye hivyo, na ampe mwaliko mumewe wa kutokosa kuhudhuria katika mnasaba huo. Aidha mwanamume naye anaweza kumualika mkewe katika hoteli ya heshima mlo wa mchana au usiku na kupata nafasi ya kujikumbusha mambo mazuri yaliopita.
g-    Kubadilisha mpangilio wa nyumba: Wanawake wengi huwalalamikia waume zao kwa kutopenda kukaa nyumbani na badala yake kumaliza muda wao kwenye migahawa na kwa marafiki zao. Mke mwerevu huwa anafanya kila juhudi za kumnasa mumewe apende kukaa nyumbani wakati wa nafasi yake kwa kumbadilishia mazingira ya nyumba, kwani mazingira ya nyumba yanapokuwa ni yale yale tangu ndoa ilipofungwa hadi wanakuwa na watoto watatu, kochi lipo palepale kama kisiki cha mti, saa ya ukutani tangu imetundikwa mpaka imeshikana na ukuta, mapazia yaleyale na kama yanabadilishwa basi rangi ni zilezile, hali hii humfukuza mwanamume ndani ya nyumba na kumfanya arudi kuja kulala tu, na huu ndio mwanzo wa kuchokana na kuichoka nyumba.
h-    Usafi wa mwili na mavazi:Moja miongoni mwa mambo yanayokera kwa wanandoa ni uchafu wa mmoja wao, uchafu ni sifa isiyovumilika hususan kwa mwanamke, baadhi ya wanawake hudhani kuwa manukato, vipodozi ndio usafi, utakuta anapitisha masiku bila kuoga kikamilifu, bali anapitisha pitisha maji na sabuni tu katika maeneo fulani, kisha kujijaza manukato, lotion na mafuta mengine, bila kuelewa kuwa, anapokuwa karibu zaidi na mumewe harufu ya asili hujitokeza na kuleta mchanganyiko wa harufu mbaya, hali kama hii si rahisi kwa mwanaume mstaarabu kuizungumzia kwa mkewe, atakaa nayo na atavumilia, lakini mwisho wake ni kumchoka mke huyu. Wanaume nao hudhani kuwa kwao wanaume ndio wamepewa kibali cha kuwa wachafu, kwa mfano wanaume wengi huona ni jambo la kawaida kunuka jasho, na wengine wana matatizo sugu ya kunuka miguu, huu ni uchafu ambao hauvumiliki kwa mwanamke msafi, aidha baadhi ya wanaume hawana vionjo katika mavazi yao, na jinsi wanavyojiweka, jambo ambalo linaweza kumsababishia mke maudhi, na hata kujihisi aibu kunasibishwa na mume wake.
i-       Kufanya Ibada za Sunnah kwa pamoja: Nguzo muhimu na     mhimili wa maisha ya ndoa ni kumcha Allaah, Swalah za usiku humkurubisha  mja karibu zaidi na Allaah, hivyo mume na mke kuhimizana kufanya  ibada hii pamoja huwazidishia imani na mapenzi baina yao na kuifanya ndoa yao kuwa imara zaidi, aidha hata funga za Sunnah za Jumatatu na Alkhamiys ni vema mume na mke wakazifunga pamoja kama hali itaruhusu hivyo. Na ni vema wakaweka katika kalenda yao  ya mwezi au miezi kwa mujibu wa nafasi zao, kutembelea Ndugu wa nasaba, kutembelea Majirani, kutembelea wagonjwa Hospitali, kutembelea Vituo vya Watoto Yatima, kujitolea katika Taasisi za Kiislamu kwa kufanya kazi au kutoa ujuzi walionao. Ibada hizi zitawazidishia imani yao na kuwafanya wawe karibu na Allaah na wawe karibu na ndoa yao.
Imeandikwa na; Shams Elmi (Abu ‘Ilm)
Chanzo Al hidaya

No comments:

Post a Comment